Thursday, 3 December 2015

na Erasto T. Ching’oro, Msemaji - Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto
Wadau wa Asasi za Kiraia (AZAKi) walishiriki Tamasha la kumi na tatu lilioanza tarehe 1- 2 Desemba 2015 katika ukumbi wa Blue Pearl jijini Dar es salaam na kufunguliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia an Watoto Bibi Sihaba Nkinga.

Mgeni rasimi Bibi Sihaba Nkinga, ametoa shukrani kwa shirika la the Foundation for Civil Society kwa kuandaa Tamasha hilo lenye Kauli Mbiu: Wajibu wa Asasi za Kiraia katika Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030’.

Ameeleza kufurahishwa na ari ya wadau wa AZAKi katika kuendelea kushiriki na kuchangia jitihada za kuleta maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla. Ameongeza kuwa kauli mbiu ya Tamasha la mwaka 2015 ni ushahidi tosha kuwa AZAKi na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ni wabia muhimu katika maendeleo
.
Akimkaribisha mgeni rasimi, Bibi DKT. Stigmata Tenga ambaye ni Rais wa Foundation for Civil Society alibainisha malengo ya Tamasha kuwa ni kutoa fursa kwa washiriki kujadili  na kuainisha masuala yatakayozingatiwa na jinsi ya kuimarishsa ushiriki wa wananchi na Asasi za Kiraia (AZAKi) na kuyapa kipaumbele wakati wa utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu. Aidha, Tamasha hilo litajenga jukwaa  kwa wadau wa AZAKi kujadili namna ambavyo Foundation for Civil Society itaboresha huduma za kujenga uwezo wa Asasi za Kiraia nchini kwa kutoa katika kuimarisha uwezo na huduma za asasi kiutendaji na kiutawala.

Tamasha la Azaki linakutanisha takribani wadau 300 kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini. Bibi Nkinga amaeleza kuwa fursa hii itatumiwa na wadau kujenga uelewa wa pamoja kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu na kuweka mikakati ya kukuza ushiriki katika utekelezaji wa malengo hayo kwa kuzingatia misingi ya uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa jamii. Amewataka wadau kushiriki katika kuandaa  Malengo  Mapya ya Maendeleo endelevu ya mwaka 2030 kusaidia kuwafahamisha wananchi mchakato uliotumika kuandaa Malengo hayo na utekelezaji wake ili kuondoa umasikini kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine.

Akifafanua Bibi Sihaba amewataka wadau kutumia Tamasha la Azaki kujadili  mafanikio na  changamoto zilizopo katika utekelezaji wa Malengo ya Milenia. Kwani majadaliano yao yataweka kuwa na uelewa wa pamoja na kuibua mipango thabiti ya utekelezaji.

Itakumbukwa kwamba, baada ya kutolewa kwa Malengo ya Maendeleo ya Milenia yaliyopita, nchi iliandaa mikakati ya kuitekeleza. Mikakati hiyo ni pamoja na MKUKUTA (Tanzania Bara), MKUZA kwa Zanzibar na Mpango wa Maendeleo wa Miaka 5. Mikakati hii ilikuwa na vipaumbele pamoja na viashiria vya kupima mafanikio na ufuataliaji ili kufikia Malengo yaliyowekwa.

Katika utekelezaji wa Malengo ya Milenia kama nchi tuliweza kupata mafanikio makubwa katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na:
kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa  mashuleni; kuongezeka kwa Idadi ya wanawake  katika vyombo vya maamuzi  kama Bunge hadi kufikia Asilimia 30; ongezeko la uwiano wa wanafunzi wa kike na wakiume katika shule za Msingi na shule za Sekondari; kupunguza kwa  Asilimia 70 (2/3)  vifo vya watoto wenye umri chini ya miaka 5; na kupungua kwa vifo vya mama na mtoto. Mengine ni kupungua kwa kiwango cha maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa watu wenye umri kati ya miaka 15-24 na 25-49; na kuongezeka kwa idadi ya wananchi wanaotumia maji safi na salama ya kunywa. Katibu mkuu Bibi Nkinga amaeleza kuwa mafanikio haya yamefikiwa kwa ushirikiano thabiti wa AZAKi na Serikali.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa Foundation For Civil Society Bw. Francis Kiwanga alieleza kuwa Tamasha la AZAKi 2015 litakuwa na mada  nne ambazo ni: wajibu  na mikakati  ya kuimarisha ushiriki wa  asasi za kiraia katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu; wajibu wa sektab binafsi katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu; wajibu wa Serikali katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu; na utunishaji mfuko na ugharamiaji wa Mpango wa Maendeleo endelevu. Rai imetolewa kuzingatia upatikanaji wa rasilimali kutoka  ndani na nje ya nchi katika kutekeleza Malengo Endelevu ya Maendeleo.

Katibu Mkuu Nkinga amebainisha kuwa, yeye anaamini kuwa bila Asasi za Kiraia makini zenye uzalendo zinazotanguliza maslahi ya taifa hatutaweza kuwa na Tanzania tunayohitaka miaka ijayo. Hivyo katika mijadala mnatakiwa kuzingatia wajibu mkubwa wa AZAKi kwa jamii katika kuchangia kufikiwa kwa malengo ya maendeleo endelevu, tunapaswa kupitia upya dhamira zetu na kuwa tayari kujifunza kwa wengine ili kuimarisha utendaji wa Asasi zetu na kutoa mchango unaokusudiwa. Washiriki wamekumbushwa kufanyakazi kazi kwa juhudi na maarifa ili kuunga mkono dhamira ya Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuwawezesha Watanzania kujiletea maendeleo yao na kuondokana na umasikini kupitia kauli mbiu  ya HAPA KAZI TU!

Watendaji wa AZAKI wametakiwa kuongeza uwazi na uwajibikaji kwa wadau mbalimbali hususan kwa jamii, serikali, wanachama na wafadhili. Utamaduni huu ukiendelezwa sio tu kwamba wadau wa Asasi za Kiraia watajijengea uhalali kwa wananchi na jamii bali pia wataweza kuimarisha ubia na Serikal.

Mwisho, Katibu Mkuu Bibi Nkinga aliwataka wadau wa Asasi za Kiraia kurejea maneno ya Muasisi wa Taifa Letu Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutoka katika Kitabu chake  cha ‘Uhuru na Maendeleo’  ambaye aliwahi kusema: "Mtu anaendelea ikiwa uwezo wake umekua au kipato chake kimeongezeka kumwezesha yeye na familia yake kuishi maisha bora zaidi; Mtu haendelei kwa kutegemea kupewa vitu na watu wengine” (1973).



0 comments:

Post a Comment