Friday, 2 October 2015

Kutokana na jitihada za Serikali za kuweka mazingira wezeshi kupitia uratibu na uwezeshaji wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, mashirika haya yameendelea kutambuliwa na wadau katika ngazi mbalimbali. Mipango mbalimbali ya kitaifa kama vile Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania - II (MKUKUTA - II) na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/2012 – 2015/16) inayatambua mashirika haya kuwa wadau muhimu katika uandaaji na utekelezaji wake. Aidha, Sera zote za kisekta hapa nchini zinayatambua Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuwa wadau muhimu katika uandaaji na utekelezaji wa Sera husika. Katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yamekuwa washiriki muhimu katika uandaaji na utekelezaji wa sera mbalimbali zikiwemo: Sera ya Afya (2007), Sera ya Elimu na Mafunzo (1996), Sera ya Maji (2000), Sera ya Mazingira (2000), Sera ya Maendeleo ya Jamii (1996), Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia (2000) and Sera ya Maendeleo ya Mtoto (2008).

Katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne Wizara, Idara na Wakala mbalimbali za Serikali na Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Majiji zimeendelea kuwa na ubia na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika utekelezaji wa Sera mbalimbali za kisekta na Kitaifa. Ubia huo ulijikita katika maeneo ya kukuza uelewa na ushiriki wa jamii katika maendeleo, ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa miradi ya Serikali, utoaji wa huduma kwa jamii, uandaaji na mapitio ya mipango na Sera mbalimbali.

Juhudi za Serikali zimesaidia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kutoa mchango katika nyanja mbalimbali za maendeleo. Kwa mujibu wa Taarifa ya Mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2012, mashirika haya yaliwekeza kiasi cha shilingi 524.5 bln katika maeneo ya elimu, afya na Virusi Vya UKIMWI/UKIMWI, maendeleo ya jinsia na utawala bora, mazingira, kinga ya jamii, maji na kilimo.

Wizara kupitia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yametoa mchango katika kutengeneza nafasi za ajira na fursa ya kujitolea kwa Watanzania. Taarifa ya Mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika Maendeleo ya mwaka 2012 inaonesha kuwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yaliajiri watu 33,388 na watu 27,312 walifanyakazi kwa kujitolea. Kati ya hao, watanzania walioajiriwa walikuwa 32, 279 na watanzania 22,996 walipata fursa ya kujitolea katika mashirika mbalimbali.


Katika Sekta ya Afya mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ulikuwa katika  maeneo mbalimbali ikiwemo matibabu kwa wanawake wenye matatizo mbalimbali hususan fistula. Mashirika Yasiyo ya Kiserikali  kupitia programu ya utengamao inatolewa na Shirika Lisilo la Kiserikali la CCBRT limeongeza uelewa kwa jamii kuhusu matibabu ya fistula kwa akinamama kuwa fistula inatibika hospitalini. Uelewa huu umewezesha wakinamama wenye matatizo ya fistula itokanayo na uzazi kwenda hospitali na kupata matibabu. Hospitali zinazotoa huduma ya Fistuli ni pamoja na hospitali ya Seliani (Arusha), KCMC (Kilimanjaro), Kabanga (Kigoma) na CCBRT, Dar es Salaam.  Katika kipindi cha 2013 hadi 2014, jumla ya wanawake 868 wamepatiwa matibabu ya fistula itokanayo na uzazi. Aidha, Programu ya utengamao inajumuisha kituo maalumu cha kuwapatia ujuzi wanawake waliotibiwa fistula itokanayo na uzazi. Kituo hiki kinaitwa “Mabinti” kiko jijini Dar es Salaam. Ujuzi unaotolewa na kituo ni pamoja na ufundi cherahani; ufumaji; utengenezaji wa urembo na mapambo kwa kutumia shanga; na  utengenezaji wa mikoba mbalimbali kutokana na mabango ya plastiki. Programu hii imewawezesha wanawake waliokuwa na matatizo ya fistula kuweza kujumuika katika jamii iliyokuwaimewatenga na hatimaye kujitegemea kiuchumi.
Mheshimiwa Anne  Semamba Makinda, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipotembelea CCBRT mwaka 2011 akiangalia baadhi ya vitu vilivyotengenezwa na wanawake waliotibiwa Fistula ambao walipata mafunzo kutoka Kituo cha Mabinti.

0 comments:

Post a Comment