Tuesday, 29 September 2015

Serikali inayatambua Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) kuwa ni wadau muhimu katika kupanua uhuru wa kujumuika na kuchangia katika maendeleo ya jamii na taifa.  Katika kipindi cha awamu ya nne, Serikali iliendelea kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya ushiriki wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika maendeleo na kukuza demokrasia na madaraka kwa umma. Juhudi hizi za Serikali zilifanyika kwa kuzingatia Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo Kiserikali na Sheria ya Mashirika Yasiyo Kiserikali Na.24 ya mwaka 2002 iliyorekebishwa mwaka 2005. Katika eneo hili la utekelezaji,  Serikali ilijikita katika usajili, uwezeshaji na uratibu wa Mashirika Yasiyo Kiserikali.

Usajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali

Serikali iliendelea kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya kupanua uhuru wa wananchi kujumuika kupitia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa kuyatambua kupitia usajili chini ya Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali  Na.24 ya mwaka 2002 kama ilivyorekebishwa mwaka 2005. Mwaka 2005 Serikali ilianza kutoa huduma za usajili chini ya Sheria ya Mashirika Yasiyo Kiserikali Na.24 ya mwaka 2002 iliyorekebishwa mwaka 2005 ambapo hadi kufikia Juni, 2014 jumla ya mashirika 6,679 yalikuwa  yamepatiwa usajili. Kati ya hayo, mashirika 5,835 yalipatiwa Cheti cha Usajili na mashirika 844 Cheti cha Ukubalifu.

Katika kusogeza huduma za usajili karibu na wananchi, mwaka 2010 Wizara iliwateua Maafisa Maendeleo ya Jamii wa ngazi ya Mkoa, Halmashauri za Miji, Wilaya, Manispaa na Majiji kuwa Wasajili Wasaidizi wa Wilaya na Mikoa husika. Aidha, Wizara ilitoa mafunzo kuhusu uratibu na usajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa maafisa hao kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara ili kuboresha huduma za usajili na uratibu. Mafunzo hayo yameongezea uelewa wa maafisa husika hivyo kuwajengea uwezo wa kuwezesha hatua za awali za usajili.

 

Uratibu na Uwezeshaji wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali

Kwa kutambua mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika maendeleo na ustawi wa jamii na taifa kwa ujumla, Serikali imekua ikichukua hatua mbalimbali za kuongeza ushiriki na kuweka mazingira wezeshi kwa mashirika haya ili kutoa mchango mkubwa katika kuondoa umasikini katika jamii. Hatua hizo ni pamoja na: kuhamasisha ubia baina ya Serikali na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali; kuimarisha mawasiliano na upatikanaji wa taarifa za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali; kutoa elimu ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2001 na Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Na.24 ya mwaka 2002; kuimarisha uwazi, uwajibikaji na mifumo ya kujitawala miongoni mwa NGOs; na kutambua mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika jamii.

Katika kukuza uwajibikaji na fursa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kujitawala, mwaka 2008 Serikali ililiwezesha Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuandaa Kanuni za Maadili ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Kanuni hizi zilitangazwa kwenye Gazeti la Serikali (Taarifa ya Kawaida Na.363) la tarehe 5 Desemba, 2008. Kanuni hizi pia zilitafsiriwa katika lugha ya Kiswahili ili kurahisisha matumizi yake kwa ajili ya kuyawezesha mashirika hayo kujitawala. Jumla ya nakala 6,500 za Kanuni hizi zilisambazwa kwa wadau kutoka katika Serikalini na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa kipindi mwaka 2009 hadi 2014.

Wizara imeendelea kuboresha mazingira kwa ajili ya kukuza ubia na uwazi katika Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Hii ni pamoja na kuhamasisha ubia katika maendeleo na uandaaji wa Sera za Kitaifa na kisekta miongoni mwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Mikutano baina ya Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na wadau imeendelea kufanyika katika ngazi ya mikoa ikitumika kuhamasisha ubia katika ngazi mbalimbali za utendaji.

Serikali kupitia Wizara YA Maendeleo Ya Jamii Jinsia na Watoto imeendelea kuwezesha upatikanaji na ubadilishanaji wa taarifa za NGOs kwa wadau. Hii ni pamoja na kuanzisha na kuendesha Tovuti ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (http//www.tnnc.go.tz) na Benki ya Taarifa na Takwimu za Uratibu wa NGOs ambapo jumla ya wadau 30,679 walinufaika na huduma hii katika kipindi cha kuanzia mwaka 2005 hadi kufikia mwaka 2014. Taarifa hizo ziliwawezesha wadau kutoka Serikalini, Taasisi za Elimu ya Juu na Utafiti, Taasisi za Fedha hususan mabenki na Wabia wa Maendeleo  kufanya maamuzi sahihi katika masuala yanahusiana na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

Bibi Gizere Hamisi Mwenye Umri wa Miaka 78 Kutoka katika Kijiji cha Ngasemi Kata ya Ubetukahe, Wilaya ya Rombo akiwa na Mtoa Huduma za Kisheria Kutoka Shirika Lisilo la Kiserikali (AJISO). Kutokana na huduma hii  Bibi Gizere Ambaye ana Watoto wa Kike tu Amewezeshwa Kumiliki eneo la Ardhi hii baada ya Kuachana na Mume wake.
Katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne, Wizara kupitia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ikiwemo AJISO yametoa elimu kuhusu Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999 na kutoa huduma za kisheria kwa wanawake ambao waliipoteza kutokana na vikwazo vya kimila. Aidha, Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yamewawezesha wasichana waliokuwa wakifanyakazi zisizo za kistaha hususan wafanyakazi wa majumbani kupata elimu ya fani mbalimbali na kuwapatia vifaa vya kuwawezesha kujiajiri na kuajiri wenzao.  Vilevile, AJISO na wadau wengine wametoa msaada wa kisheria kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

Mchango wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yanayoratibiwa na Wizara ikiwemo CCBRT  yamewezesha watoto wenye mahitaji maalum wakiwemo wenye ulemavu wa viungo kuandikishwa katika shule na kupata elimu. CCBRT pia imetoa mafunzo kwa walimu na wazazi kuhusu haki za watoto kupata elimu. Pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu na wazazi pia huwapatia watoto wenye ulemavu wa viungo viti maalumu na madawati maalumu kulingana na ulemavu walio nao. CCBRT imeendelea kutoa elimu kwa walimu na wazazi kuhusu miundombinu rafiki ikiwa ni pamoja na vyoo, madarasa na mazingira ya shule kwa ujumla. CCBRT imewafundisha wanafunzi kuhusu ulemavu na namna ya kuwasaidia wenzao wenye ulemavu wakiwa shuleni na nyumbani. CCBRT imewalipia ada ya shule na usafiri watoto wenye ulemavu ambao wazazi wao hawana uwezo. Katika kipindi cha 2005 hadi kufikia 2014 jumla ya watoto 477 wenye ulemavu mbalimbali walikuwa shule za msingi jijini Dar es Salaam kuanzia 2005 mpaka 2014. Kati yao watoto 173 mpaka 2014 waliweza kumaliza Elimu ya Msingi na watoto 17 walichaguliwa kuendelea na Elimu ya Sekondari. Vilevile, CCBRT imetoa huduma ya utengamao kwa wanawake wenye fistula na watoto wenye ulemavu.


0 comments:

Post a Comment